Kwa mujibu wa Idara ya tarjuma ya Shirika la Habari la Hawza, mamluki na wanamgambo wanaohusishwa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Bahrain, kwa kuweka mzingiro mkali wa kiusalama katika “mji wa Al-Diraz”, ulioko magharibi mwa Manama, wamezuia kufanyika Swala ya Ijumaa kwa Mashia wa Bahrain kwa wiki ya 77 mfululizo.
Mamluki hao wameimarisha uwepo wao katika maeneo yanayouzunguka “Msikiti wa Imam Sadiq (as)”, wakisaidiwa na magari ya kijeshi pamoja na vikosi vyenye silaha. Hatua hiyo imechukuliwa kwa lengo la kukabiliana na uwezekano wa kuanza kwa maandamano ya wananchi kupinga mzingiro wa kiusalama na kidini dhidi ya ibada za kidini za Mashia, pamoja na kuwaunga mkono wanazuoni mashuhuri wa Kishia walioko kizuizini.
Licha ya mzingiro huo wa kiusalama, maeneo mengi ya Bahrain yalishuhudia maandamano ya wananchi wakitaka kuachiliwa wafungwa na kuachiwa mara moja wanazuoni wa dini pamoja na wafungwa wa mapinduzi wa Kishia. Waandamanaji pia walilaani hatua ya utawala unaotawala ya kuzuia kufanyika kwa ibada za Swala ya Ijumaa.
Waandamanaji walisisitiza kupinga kwao utawala rasmi juu ya masuala ya kidini na vizuizi vinavyoendelea dhidi ya uhuru wa kidini. Walitaka kukomeshwa kwa mzingiro dhidi ya ibada za kidini za Mashia, kusitishwa mashambulizi dhidi ya watu mashuhuri, wanazuoni wa dini, taasisi na misingi ya madhehebu ya Jaafaria, pamoja na kukomeshwa sera za unyanyasaji wa kimadhehebu na ubaguzi wa rangi dhidi ya Mashia.
Aidha, waandamanaji walielezea kupinga uwepo wa kijeshi wa Marekani katika ardhi ya Bahrain na kusisitiza mshikamano wao kamili na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Mhimili wa Muqawama katika vita vya kuzuia mashambulizi ya Marekani na Wazayuni pamoja na vitisho vya kiusalama katika eneo hilo.
Walitaka kuondoshwa kambi za kijeshi za kigeni ili kufikia mamlaka kamili na usalama nchini. Zaidi ya hayo, walisisitiza kukomeshwa mchakato wa kuhalalisha uhusiano na utawala wa Kizayuni, kukatwa uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi na utawala huo, kufukuzwa balozi wa utawala huo nchini Bahrain na kufungwa kwa ubalozi wake mjini Manama.
Maoni yako